Jumamosi, 15 Julai 2017

VIJIJI 347 KUPATA UMEME ITILIMA



  Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Mhe.Dkt.Medard Kalemani akizindua Mradi wa Umeme Vijijini (REA)Awamu ya Tatu Mkoani Simiyu katika Kijiji cha Nangale wilayani Itilima (kushoto) Mkuu wa mkoa huo, Mhe.Anthony Mtaka.

NAIBU Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani amezindua Mradi
wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu (REA III) katika Mkoa wa Simiyu ambapo
vijiji 347 mkoani hapo vipata nishati hiyo.

Uzinduzi  huo ulifanyika juzi katika Kijiji cha Nangale ,Kata ya
Ndolelezi wilayani  Itilima na kuhudhuriwa na viongozi
mbalimbali wa Serikali, Wabunge na wananchi wa mkoa wa Simiyu.


Naibu Waziri alitaja lengo jingine la REA III kuwa ni kupeleka umeme
kwenye vijiji vyote ambavyo havijapata umeme sambamba na hayo
alibainisha malengo mengine kuwa ni kupeleka umeme kwenye Taasisi zote
za umma na nyingine zilizo rasmi hata kama siyo za umma.

“Taasisi hizo ni pamoja na Vituo vya Afya na Zahanati, Shule pamoja na
Taasisi nyingine muhimu pia kwenye miundo mbinu ya maji ambayo ni
mitambo ya maji,” alifafanua.

Akizungumza na wananchi  mara baada ya uzinduzi, Dk Kalemani
alibainisha malengo ya REA III ambapo alisemaa lengo la kwanza la
Mradi huo kabambe ni kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote .

“Katika Mradi wa REA II tulikuwa tunapeleka umeme katika Kituo tu cha
Kijiji, siyo Kijiji chote  REA III itafika katika vitongoji
vyote.”alisema huku akishangiliwa na wananchi waliohudhuria hafla
hiyo.
 
Baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Itilima wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Mhe.Dkt.Medard Kalemani(hayupo pichani) wakati wa wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Umeme Vijijini (REA)Awamu ya Tatu Mkoani Simiyu katika Kijiji cha Nangale wilaya ya Itilima.

Pia aliwashukuru wananchi kuitikia Mradi huo wa Serikali ambao
alibainisha kuwa utatekelezwa ndani ya kipindi cha miaka minne ambapo
katika awamu ya kwanza mradi huo utatekelezwa katika vijiji 152 kwa
kipindi cha miezi 24 na vijiji vingine vilivyobaki 195 navyo
vitapatiwa umeme kwa kipindi kingine cha miezi 24.

Hata hivyo aliwataka wananchi kuutumia umeme watakaounganishiwa
katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.

“Tunapenda sana umeme huu utumike kwenye shughuli za kilimo hususan
kilimo cha umwagiliaji, kuendeshea mitambo ya maji, lakini hata
kuanzisha viwanda vya kati ili kukuza uchumi wetu tunaamini kuwa umeme
huu utakuwa kichocheo kikubwa katika kusukuma maendeleo,” alisisitiza.

Vilevile, Naibu Waziri alibainisha kuwa lengo la Serikali ni kuwapatia
wananchi wote umeme pasipo kubagua aina ya makazi wanayoishi.

“Mahali popote mwananchi anapoishi, ndipo tutakapomtundikia umeme.
Hatutajali ni nyumba ya nyasi au ya ghorofa.”alisema

Kupitia uzinduzi huo, Naibu Waziri aliwatambulisha kwa wananchi na
viongozi wa mkoa  Wakandarasi wawili  ambao ni White City
International Contractors na Guang Dong Jianneng Electiric Power
Engineering Co Ltd watakaotekeleza Mradi huo ili kurahisisha
ufuatiliaji wa utekelezaji wa kazi zao pamoja na kuwapatia ushirikiano
stahiki.

Dkt Kalemani alitoa angalizo kwa Wakandarasi hao na kuwataka kuwatumia
wakandarasi wasaidizi wenye uwezo waliko ndani ya Mkoa wa Simiyu huku
akipiga marufuku kuingiza nguzo na transfoma kutoka nje ya nchini
sambamba na Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) kuwasimamia katika kazi
Usiku na Mchana ili kuhakikisha kuwa mradi huo unaisha kwa wakati
uliopangwa.

Awali, akitoa hotuba ya utangulizi katika hafla hizo za uzinduzi,
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Gissima
Nyamo-Hanga aliwataka wananchi watakaounganishiwa umeme kukamilisha
utandazaji wa nyaya katika nyumba zao mapema ili mkandarasi
atakapofika katika maeneo yao wawe tayari kulipia na kuunganishiwa
umeme.

Aidha alibainisha kwamba kwa nyumba ambazo utandazaji wa nyaya utakuwa
haujakamilika, wananchi wanaweza kuomba kufungiwa kifaa cha Umeme
Tayari (UMETA) ambacho hakihitaji nyumba nzima kutandazwa waya.

Mhandisi Nyamo-Hanga aliwaomba watendaji katika Serikali za Kata na
Vijiji, kubainisha maeneo maalum ya viwanda ambayo katika mradi huo
yatafikishiwa miundombinu ya umeme mkubwa ili kuwezesha wajasiriamali
vijijini kupatiwa umeme utakaowezesha kuanzishwa kwa viwanda vidogo
vidogo na vikubwa vijijini kwa gharama nafuu.

Gharama ya utekelezaji wa Mradi wa REA III kwa Mkoa wa Simiyu ni
shilingi bilioni 33.47.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni