Ijumaa, 28 Julai 2017

RC; SIMIYU YAJIPANGA WAFUGAJI WAFUGE KISASA

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe, .Anthony Mtaka akizungumza na viongozi wa Serikali, viongozi wa dini, wafugaji,wataalam na wadau mbalimbali wa mifugo kutoka ndani na nje ya Simiyu(hawapo pichani) katika kikao maalum kilichofanyika Mjini Bariadi.



SERIKALI Mkoani Simiyu yajipanga kwa kuweka mkakati utakaowasaidia wafugaji mkoani humo kufugaji  kisasa kwa ufugaji wenye tija.


Aidha imedhamiria kuwatambua wafugaji wote, maeneo yao na kuwaelemisha kuhusu upimaji wa maeneo hayo ili wayatumie kufuga kisasa badala ya kuhama hama kufuata maji na malisho katika mikoa mingine.

 Serikali mkoani hapo kupitia wataalam wa kilimo na mifugo watatoa elimu kwa Wafugaji watakaorasimisha maeneo yao, ili wayatumie kupata malisho ya mifugo na kuweka miundombinu muhimu ya mifugo kama majosho na visima katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa malisho na maji.


Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu katika kikao maalum ambacho kimewahusisha viongozi wa Serikali, viongozi wa dini, wafugaji,wataalam na wadau mbalimbali wa mifugo kutoka ndani na nje ya mkoa  kilichofanyika katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Bariadi.


“Hatuwezi kuwa Serikali ambayo ina majibu mepesi kwenye mambo ya msingi,lazima tupate majawabu ya wafugaji ndani ya mkoa wetu, tufike mahali ambapo mfugaji kutoka mkoa wa Simiyu hatapigwa faini kwenye mikoa mingine kwa sababu ya kutafuta maji na malisho”amesema Mtaka


Aliongeza kuwa Mkoa unaandaa utaratibu ambapo shule za Serikali zitakapokuwa zinafungwa, idara ya kilimo na mifugo itatumia madarasa hayo kutoa elimu ya ufugaji na kilimo bora kwa wananchi.

Hata hivyo  alisema zoezi la kupima maeneo ya wafugaji na kuweka miundombinu muhimu ya mifugo litakapokamilika Serikali imepanga kuweka mizani katika minada yote mkoani humo ili wafugaji wasidanganywe na kuibiwa wanapouza mifugo yao.


Kwa upande wake Daktari wa Mifugo wa Sekretarieti ya Mkoa wa Simiyu, Gamitwe Mahaza alisema baadhi ya wafugaji  ni wakulima, hivyo ni vema wakatumia masalia ya mazao kwa ajili ya malisho badala ya kuyaacha mashambani huku  akasisitiza juu ya urasimishaji wa maeneo yao ili miundombinu kama visima iwekwe kusaidia ukuaji wa malisho ya asili na upandaji wa malisho ya kisasa.

Naye Mtaalam wa Mifumo ya TEHAMA kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia(COSTEC), Mhandisi George Mulamula ameeleza kuwa upimaji katika maeneo ya wafugaji unaweza kufanyika kwa kutumia njia mbalimbali zikiwemo zinazotumia mifumo ya TEHAMA , kama vile matumizi ya satelite na ndege zisizotumia rubani  ambazo zitasaidia zoezi hilo kufanyika kwa haraka.



Mkoa wa Simiyu ni moja ya mikoa inayoongoza kwa kuwa na mifugo mingi hapa nchini, hali inayopelekea baadhi ya wafugaji kuhamia maeneo mengine ili kutafuta malisho, hivyo Serikali imedhamiria kuona wafugaji mkoani humo wanahama kutoka kwenye kufuga kwa mazoea na kuingia kwenye ufugaji wa kisasa wenye tija.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu akichangia jambo katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa ufugaji bora Mkoani Simiyu, kilichofanyika Mjini Bariadi katika Ukumbi wa kanisa Katoliki.

Baadhi ya viongozi wa Serikali, wafugaji,wataalam na wadau mbalimbali wa mifugo kutoka ndani na nje ya Simiyu wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika kikao maalum kilichofanyika Mjini Bariadi, kujadili juu ya mkakati wa ufugaji bora 
Na ANITA BALINGILAKI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni