Jumapili, 9 Julai 2017

MBUNGE AIOMBA WIZARA YA AFYA WATUMISHI, VIFAA TIBA.


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiongea na wananchi wa kata ya Nkoma na wilaya ya itilima mara baada na kuwahakikishia kuwa mwezi Desemba wataleta mashine ya Mionzi (ultra sound) katika kituo hicho.


MBUNGE wa Jimbo la Itilima Njalu Silanga ameiomba wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kuhakikisha inaleta wataalamu wa idara ya afya ili kuweza kutoa huduma stahiki katika jengo la upasuaji kata ya Nkoma lililofunguliwa juzi na Rais mstaafu Mkapa.

Njalu alisema kuwa pamoja na kukamilika kwa jengo hilo upungufu wa watumishi bado ni changamoto kubwa na wajibu wa serikali ni kuajiri watumishi ili waweze kuhudumia wananchi kwa mujibu wa sera ya afya .

Aliyasema hayo juzi wakati Taasisi ya Mkapa foundation ikikabidhi jengo la upasuaji katika kata ya Nkoma wilayani Itilima mkoani simiyu ili kunusuru maisha ya wagonjwa ambao awali hawakuwa na huduma hiyo ya upasuaji.


‘’nikuombe mheshimiwa waziri wa afya kuhakikisha unaangalia upatikanaji wa wataalamu ili wakinamama hawa waweze kujifungua salama…lakini pia tutashirikiana na wananchi kuhakikisha tunatunza miundombinu iliyowekwa hapa ili iweze kudumu kwa kushirikiana na wataalamu’’ alisema Njalu.

Aliongeza kuwa wilaya ya Itilima ina vituo vya afya vitatu na zahanati 23 lakini watumishi wa idara hiyo wamekuwa hawakidhi mahitaji  ya wananchi wanaofika kupata huduma.
Mbunge wa Jimbo la Itilima Njalu Silanga akiwapongeza taasisi ya Mkapa foundation kwa kujenga na kukabidhi jengo la Upasuaji kata ya Nkoma wailayani Itilima Mkoani Simiyu jana.


Kwa upande wake waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu alisema  kufikia  Desemba mwaka huu   serikali italeta mashine ya ultra sound ili kuweza kukidhi mahitaji ya wagonjwa, na pia wataajiri zaidi ya watumishi wa afya 3000 na kupunguza changamoto ya uhaba wa watumishi wa afya.


Mwalimu alisema kuwa serikali itaendelea kutatua changamoto za afya hasa huduma ya upasuaji ili kufuikia 2020 angalau 50% ya vituo vya afya vitoe huduma ya upasuaji ili kuokoa maisha ya wagonjwa.
Aliongeza kuwa vifo vitokanavyo na uzazi kati ya wakina mama 100,000 vimepungua kwa mwaka hadi 559 kwa mwaka ambavyo husababishwa na kuvuja damu, maambukizi ya maradhi na uzazi pingamizi.

Katika hatua nyingine Mwalimu amesema kuwa serikali imetoa bei elekezi kwa dawa za binadamu ili hata mwananchi mwenye kipato kidogo aweze kumudu gharama za matibabu huku akisisitiza kuwa dawa siyo bure.


“Hatutoi  dawa bure na wananchi mnatakiwa kuchangia dawa katika vituo na zahanati…bei za dawa zimepunguzwa tunataka wananchi waone upungufu huo ” alisema Mwalimu.


Jengo hilo ambalo limejengwa na taasisi ya Mkapa Foundation kwa kushirikiana na nchi ya Japan limegharimu milioni 270 ambapo litaweza kuhudumia wakinamama wajawazito wenye uzazi pingamizi, na wagonjwa wengine ambapo awali walikuwa wakiipata huduma hiyo umbali wa kilomita 40 katika wilaya ya Bariadi.


Wananchi waliohudhuria katika ufunguzi huo walisema kuwa jengo hili limeongeza faraja kwa akinamama wajawazito waliokuwa wakipata uzazi pingamizi na wagonjwa kwani wengi wao walikuwa wakifia njiani wakati wakisafirishwa kwenda hospitali ya Somanda kupata huduma ya upasuaji.

Ufunguzi wa jengo hilo ulihudhuriwa na Rais mstaafu wa awamu ya tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Benjamini Mkapa .

Na ANITA BALINGILAKI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni