Jumatatu, 7 Agosti 2017

RC SIMIYU:WAKUU WA SHULE KUWENI WABUNIFU


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu. Mhe,Anthony Mtaka akizungumza na Wakuu wa Shule (hawapo pichani) wakati wa kufunga mafunzo yao ya siku mbili yaliyofanyika Mjini Bariadi, (kulia) Afisa Elimu Mkoa, Mwl.Julius Nestory.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu  Anthony Mtaka amewataka Wakuu wa Shule zote  mkoani Simiyu kuongeza ubunifu ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika shule zao.
 Aidha amesema kuwa wakuu wa shule wanatakiwa kuwa wabunifu hususani katika mbinu mbalimbali zitakazosaidia kuwaandaa wanafunzi vizuri kitaaluma  ikiwa ni pamoja na mazoezi na mitihani ya kujipima ya mara kwa mara, zitasaidia wanafunzi kufanya vizuri katika mitihani ya ndani na ile ya  kitaifa.

Mtaka ameyasema hayo wakati alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili kwa wakuu wa shule zote za Sekondari yaliyofanyika Mjini Bariadi katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Bariadi

  “Kiongozi lazima uwe mbunifu, Mkiwa wabunifu kwenye shule watoto watafanya vizuri,mnapaswa kubuni mbinu na mikakati mbalimbali kwenye majaribio ya darasani, mitihani ya kujipima na  kubuni namna ya kuwapa motisha walimu wenu wapende kazi na kujiona ni wanafamilia katika shule mlizopo” alisema Mtaka.
Aidha, aliwataka wakuu hao kujiwekea utaratibu wa kupita mara kwa mara madarasani kukagua madaftari ya wanafunzi kwa lengo la kujiridhisha, ikiwa walimu wanatimiza wajibu wao wa kuwafundisha kama inavyotakiwa badala ya kusubiri kuletewa taarifa.
Mkuu huyo wa Mkoa pia aliwaasa wakuu hao kuwa na uongozi shirikishi ambao unajali pande zote kwa maana ya walimu, wanafunzi na wazazi ili waweze kujua kero na masuala mbalimbali yasiyowaridhisha na waweze kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa taratibu kuyapatia suluhu.
Hata hivyo   alisisitiza wakuu wa shule kufanya vikao na wazazi kwa kuwa wazazi wanayo nafasi kubwa ya kuchangia wanafunzi kufanya vizuri, hivyo akawataka wavitumie vikao kupata maoni ya wazazi katika masuala mbalimbali ya kuboresha maendeleo ya wanafunzi kitaaluma.
Aidha aliwataka Wakuu hao wa Shule kuzingatia sheria, kanuni , taratibu na kuchukua hatua stahiki pale inapobidi ikiwa ni pamoja na kutowaruhusu wanafunzi wajawazito au waliojifungua kuendelea na masomo.
Kwa upande wake Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl.Julius Nestory alisema katika mafunzo hayo ya siku mbili wakuu wa shule wameelimishwa juu ya sheria zote nne za Elimu, falsafa,nyaraka,kanuni mbalimbali za Elimu na sera mpya ya Elimu.
wakuu   hao walipewa mafunzo ya utunzaji wa nyaraka za Serikali, udhibiti wa vitendo vya rushwa, kusimamia shule na taaluma pamoja na utunzaji wa takwimu sahihi ambapo aliwataka wakuu wa shule hao kutumia sheria zilizopo katika kusimamia shule kupitia mipango thabiti itakayotoa matokeo chanya.
Naye Magebu Bugacha Mkuu wa Shule ya Sekondari Mwantimba ameshukuru uongozi wa Mkoa kuona umuhimu wa kuwaandalia wakuu wa shule mafunzo hayo ya kuwajengea uwezo ambayo yatawasaidia na kuwapa uzoefu katika kuendesha na kusimamia shule zao.
Jumla ya Wakuu wa shule 152 kutoka katika Halmashauri zote sita za Mkoa wa Simiyu wamepata  mafunzo hayo ambayo yalilenga kuwajengea uwezo katika usimamizi na uendeshaji wa shule za Sekondari.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu.Anthony Mtaka akizungumza na Wakuu wa Shule (hawapo pichani) wakati wakufunga mafunzo yao ya siku mbili yaliyofanyika Mjini Bariadi,(wa pili kulia Mkuu wa TAKUKURU mkoa waSimiyu, Adili Elinipenda.

Baadhi ya Wakuu wa Shule za Sekondari Mkoani Simiyu wakimsikiliza Mkuu wa mkoa huo, mhe,Anthony Mtaka (hayupo pichani)alipozungumza nao wakati akifunga mafunzo ya siku mbili Mjini Bariadi.     

Na ANITA BALINGILAKI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni