Jumatatu, 7 Agosti 2017

ARUSHA,MWANZA WANG'ARA SIMIYU JAMBO FESTIVAL

Naibu Spika wa Bunge la  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Tulia Ackson (mwenye bendera nyeupe kulia) akifungua mashindano ya Mbio za Baiskeli Mkoa wa Simiyu(Simiyu Jambo Festival) kwa kuruhusu washirikuanza mashindano hayo Mjini Bariadi.


Hatimaye Mashindano ya mbio za Baiskeli, yaliyohusisha washiriki kutoka mikoa ya Mwanza, Simiyu na Arusha yamekamilika mkoani Simiyu, huku mshiriki kwa upande wa wanaume kutoka Mkoa wa Arusha kuibuka mshindi na Mkoa wa Mwanza ukitoa mshindi wa kwanza kwa upande wa wanawake.

Mashindano hayo ambayo kwa mara ya kwanza yameandika historia kwa Mkoa wa Simiyu yalimalizika jana, huku idadi kubwa ya watu wakijitokeza kushuhudia mbio hizo za baiskeli ambazo zilianzia eneo la Salunda na kumalizikia katika viwanja vya Halmashuri ya Mji wa Bariadi.

Akizungumzia mashindano hayo, Mgeni rasmi wa mbio za baiskeli kwa mwaka 2017, Naibu Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Tulia Ackson amesema Mkoa wa Simiyu umeandika historia na kwamba mikoa mingine ijufunze kutoka Simiyu, huku akitoa wito kwa wanawake kushiriki kwa wingi kwenye michezo.

Tulia alisema kuwa michezo nchini haijapewa kipaumbele lakini ikitumiwa vizuri inaweza kutoa ajira ukiwemo mchezo wa mbio za baiskeli; ambapo ametoa wito kwa viongozi wa mikoa mingine pia kuwekeza katika michezo mbalimbali ili kuwasaidia wananchi kupata kipato.

“Lililofanyika Simiyu ni jambo jema sasa hivi watu watakuwa wanajua kuwa wakijifua vizuri kwenye baiskeli na ngoma za jadi wanakuja kushiriki mashindano ya Baiskeli na  ngoma Simiyu, nitoe wito kwa viongozi wengine kufikiria mambo mengine yanayoweza kuwasaidia wananchi katika maeneo yao kupata ajira na kujipatia kipato” alisema.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka amesema mkakati wa mkoa huo ni kurasimisha tamaduni zote na kuhusianisha na shughuli za Utalii ndani ya mkoa huo.
  
“ wasanii wote watatambuliwa na baadae kujengewa uwezo  kupitia watalaam wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(Kitivo cha sanaa),Chuo cha Sanaa Bagamoyo na vyuo vya michezo ili waweze kufanya kazi zao kibiashara na kuimarisha uchumi wao” alisema Mtaka.

Wakizungumzia ushindi baadhi ya washiriki kutoka Simiyu, Arusha na Mwanza walisema hiyo ni fursa nzuri ya kujiandaa kwa mashindano makubwa na kwamba wadhamini waendelee kujitokeza kudhamini michezo kama hiyo.

Mashindano hayo yalidhaminia na Jambo food products ambapo mshindi wa kwanza kundi la wanaume waliokimbia km 200 alijinyakulia zawadi ya pikipiki yenye thamani ya sh milioni mbili  Khamis Hussen kutoka Arusha mshindi wa pili Masunga Duba kutoka simiyu na kujinyakulia kiasi ya pesa milioni moja(1,000,000,000) na mshindi wa tatu Richard Raiza kutoka arusha ambaye alijipatia laki tano.

Upande wa wanawake mshindi wa kwanza alikuwa Laulencia Mtuba kutoka mwanza na kujinyakulia laki tano,mshindi wa pili Tatu Charles Kutoka mwanza ambaye alijipatia shilingi laki nne huku mshindi wa tatu Vumilia Msinambula kutoka simiyu na kuambuli shilingi laki tatu.

Watu wenye  walemavu waliokimbia km 5 mshindi wa kwanza Emmanuel Mtemi ambaye alijinyakulia shilingi laki mbili,mshindi wa pili Masunga Sendema ambaye alichukua shilingi laki moja na nusu,huku mshindi wa tatu Saguda Sospeter ambaye alijinyakulia shilingi laki moja.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Jambo Food Products,Mhe.Salum Khamis ambaye ndio Mdhamini wa mashindano ya Baiskeli na ngoma za Asili (Simiyu Jambo Festival) amesema ataendelea kudhamini mashindano kama hayo Mkoani Simiyu ili kuwawezesha wananchi kuinua kipato kupitia vipaji vyao.
Na ANITA BALINGILAKI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni