Jumatano, 6 Septemba 2017

RC MTAKA:SIMIYU KUJENGA KIWANDA CHA BIDHAA ZA AFYA


Mkuu wa mkoa wa Simiyu mhe, Antony Mtaka akizungumza na wananchi wa Kata ya Dutwa(hawapo pichani) Wilayani Bariadi katika Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Igaganulwa  wakati wa ziara yake aliyofanya kwa lengo la kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.


MKUU wa Mkoa wa simiyu Antony Mtaka  amewahamasisha wananchi kuendelea kulima zao la pamba kwa kuwa Serikali imekusudia kujenga kiwanda cha bidhaa za Afya zitokanazo na zao hilo mkoani humo na wataalam wanaofanya upembuzi yakinifu wanatarajia kufika Mkoani Simiyu Septemba 20 mwaka huu kuona eneo kitakapojengwa kiwanda.

Mkuu huyo amesema wananchi wasikate tamaa kulima pamba kwa sababu ya matatizo ya kihistoria na kuwaeleza, Serikali ya Mkoa imeweka  mikakati madhubuti ya kuirudisha pamba kuwa dhahabu, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata pembejeo, mbegu bora, dawa, na suala la bei ya pamba itaanza kujadiliwa mapema.

Hata hivyo amewataka  wakulima  wasiache kulima mazao jamii ya mikunde hususani choroko na dengu kwa kuwa Serikali inashughulikia suala la upatikanaji wa soko la uhakiki pamoja na kupunguza au kuondoa kabisa  madalali katika biashara ya mazao hayo ili wananchi wanufaike kupitia kilimo.

Akitolea ufafanuzi hoja ya Diwani wa Kata ya Ikungulyabashashi.Bupi Maduhu Litunga ya kupimiwa maeneo, Mkuu huyo wa Mkoa amemuagiza mkurugenzi  mtendaji wa  halmashauri ya Wilaya Bariadi kupitia Idara ya Ardhi, kuitisha mikutano katika Vijiji vyote ambavyo wananchi wanahitaji  kupimiwa maeneo na baadae awasilishe mihutasari ya vikao hivyo Ofisini kwake tarehe 13/09/2017.


Katika hatua nyingine Mtaka amepiga marufuku Halmashauri zote Mkoani humo kutoza ushuru wa biashara ndogondogo zinazofanywa na wananchi kwa kutandika na kupanga bidhaa zao chini au kuuzwa katika mabeseni maarufu kama matandiko.

Amesema suala hilo lilishatolewa maelekezo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli, hivyo Halmashauri zinapaswa kubuni vyanzo vipya vya mapato vyenye tija kwa Halmashauri badala ya kutegemea kutoza ushuru unaowakwaza wananchi.

Hata hivyo ameitaka Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi  kuhakikisha inarejesha asilimia Kumi ya mapato yanayokusanywa kutoka katika vijiji vyote kwenye kila robo mwaka ili Vijiji hivyo viweze kutekeleza mipango ya maendeleo iliyowekwa.


Mtaka ametoa agizo hilo wakati wa ziara yake wilayani Bariadi yenye lengo la kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi .


“Kama kuna Halmashauri bado inatoza ushuru wa matandiko wamechelewa sana, kuanzia kesho hamna huo ushuru, kama mnafikiri mapato ni kutoza tandiko la dagaa…mchicha poleni   kama wakuu wa idara hiki ndicho chanzo mnachokifikiria kichwani hiyo kazi haiwafai, mkatafute kazi nyingine za kufanya” alisema Mtaka.na kuongeza kuwa:

 “. Sasa mtu anahangaika na beseni lake la nyanya wewe unamtoza ushuru, umechangia nini, beseni si lako nyanya si zako” alisema Mtaka.
Mtaka amekamilisha ziara yake katika Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi ambapo amesikiliza na kutatua kero za wananchi katika sekta ya Elimu,Afya, Kilimo, Mifugo, Ardhi, Ujenzi, Biashara na Uchumi pamoja na suala la utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini (REA) ambazo amezitolea maelekezo na ameahidi kufuatilia utekelezaji wake.

Baadhi ya Wananchi wa Kata ya Dutwa wakimsikiliza wilayani Bariadi Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(hayupo pichani) katika Mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Igaganulwa wakati wa ziara yake yenye lengo la kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.


Baadhi ya Viongozi na Wataalam kutoka Mkoa wa Simiyu na Wilaya ya Bariadi wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na wananchi wa Kata ya Dutwa katika Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Igaganulwa  wakati wa ziara Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka  aliyofanya  Wilayani humo kwa lengo la kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.
 



Na ANITA BALINGILAKI


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni